UDSM WAFUNDISHWE KWA KISWAHILI- PROF. MUKANDALA. - KABONGE BLOG.

Blog hii ni kwaajili ya masuala/taarifa za kidini na matukio yanayotokea kila siku.

Breaking

Thursday, December 1, 2016

UDSM WAFUNDISHWE KWA KISWAHILI- PROF. MUKANDALA.

MAKAMU Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Rwekaza Mukandala ameshauri chuo hicho kuangalia uwezekano wa kufundisha baadhi ya masomo kwa lugha ya Kiswahili kwa kuwa inawezekana, wapo wahadhiri wengi wanaoweza kuandika vitabu kwa lugha hiyo akiwemo yeye.

Aliyasema hayo jana chuoni hapo wakati wa hafla ya kutunukiwa kwake Tuzo ya Kiswahili, iliyotolewa na Taasisi ya Taaluma za Kiswahili (TATAKI), kwa kutambua mchango wake katika kukuza lugha hiyo na kuifanya kuwa lugha rasmi ya mawasiliano chuoni na katika vikao vya baraza la chuo hicho.

Akizungumza baada ya kukabidhiwa tuzo hiyo na Balozi wa Kiswahili Barani Afrika, Mama Salma Kikwete, Profesa Mukandala alisema inawezekana kabisa kukawa na masomo yanayofundishwa kwa lugha ya Kiswahili ili kuikuza lugha hiyo.

“Mimi mwenyewe na wengine tunaandika kabisa vitabu vya taaluma katika Kiswahili, hakuna sababu kabisa kwa nini Kiswahili kishindikane kufundishwa kwa baadhi ya masomo sio yote,” alisema Profesa Mukandala na kuongeza: “Nilishangaa miaka minne iliyopita, niliombwa ruksa kwa mwanafunzi wa Uzamivu awasilishe Tasnifu yake kwa lugha ya Kiswahili, nikashangaa kwa sababu anasoma Kiswahili sasa kwa nini awasilishe kwa lugha ya Kiingereza, nilimruhusu, nikaribishe na wengine.”

Alisema tatizo lililokuwa huku nyuma ni kwamba ilipotokea kuna mkutano mikubwa inayowashirikisha wageni wasiojua lugha ya Kiswahili, walitumia Kiingereza katika mikutano hiyo na kwamba, chuo hicho kinaweza sasa kutayarisha vifaa ma mitambo ili wakalimani wavitumie kuwatafsiria wageni hao ili lugha ya Kiswahili iendelee kutumika badala ya Kiingereza.

“Vifaa hivyo viwepo Nkrumah, ili wageni hao wavitumia na wasizuie sisi kutumia lugha ya Kiswahili kwenye mikutano yetu, wao watafsiriwe kwa lugha zao na wakalimani,” alisisitiza Profesa Mukandala.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mshiriki wa Tataki, Dk Musa Hans alisema matumizi ya lugha ya kiswahili chuoni hapo ni makubwa na kila leo lugha hiyo inaimarika na kuwa na misamiati mingi na imekuwa ikutumika kama lugha ya mawasiliano, kufundishia na matumizi yasiyo rasmi.

Dk Hans alisema kupitia chuo hicho na taasisi hiyo ya Tataki, wameshasanifisha majina mengi ya misamiati kwa lugha ya Kiswahili, ikiwemo majina ya vitengo na Histilahi na sasa yatatambulika rasmi.

Kwa upande wake, Mama Kikwete alimpongeza Profesa Mukandala na uongozi wa chuo hicho kwa hatua ya kukuza lugha hiyo na kuwataka waendelee kuikuza na yeye kama Balozi wa Kiswahili Afrika atasaidia kuendeleza lugha hiyo.

2 comments:

  1. Mtizamo huo ni yakinifu kabisa
    Nikimaanisha matumizi yalugha hii yakiswahili yatakapotiliwa mkazo ,lugha yetu itaendelea kutambulika nakuthaminiwa katika kila nyanja tofauti tofauti. Tuithamini lugha hii he kiswahili sote kwa pamoja kwa utambulisho wa nchi yetu Tanzania.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Asante Agreth Stephen kwa maoni yako.

      Endelea kutembelea blog hii kwa habari zaidi.

      Delete